Silioni kosa langu kwa kufanya hivyo,
kwani Rasimu imetolewa hadharani kwa watu kuijadili. Na mimi kama raia ninayo haki ya kufanya
hivyo kama wafanyavyo wengine. Kwa nini
nilaumiwe kwa kutumia haki yangu hiyo.
Lakini, pia mimi ndiye Rais wa nchi yetu,
ninayo dhamana ya uongozi na ulezi wa taifa letu. Itakuwaje kwa jambo kubwa la hatma ya nchi
yetu nilinyamazie kimya. Watanzania
wangeshangaa na wangekuwa na haki ya kuhoji Rais wao ana maoni gani. Bahati nzuri nilitoa maoni yangu mahali
penyewe hasa, na kwa uwazi, kwenye Bunge Maalumu la Katiba. Hata hivyo, ni muhimu kusisitiza kuwa namna
nilvyotoa maoni yangu sikuwa natoa maagizo wala kushurutisha, ndiyo maana kila
wakati niliwakumbusha Wajumbe kuwa mamlaka ya uamuzi ni yao. Yangu yalikuwa
maoni tu wanahiyari ya kuyakubali au kuyakataa.
Niliwataka Wajumbe wasome na
kuielewa vyema Rasimu. Nilisema wasome
sura kwa sura, mstari kwa mstari na neno kwa neno. Niliwaomba wajiridhishe kuhusu uandishi na
dhana mbalimbali. Nilitoa mifano ya
mambo yahusuyo uandishi ambayo ni vyema wayatazame. Pia nilitoa mifano ya dhana ambazo niliwasihi
wajiridhishe juu ya kufaa kwake kuwepo.
Kuhusu muundo wa Serikali tatu, nilieleza wazi kuwa sina tatizo nao kama
ndiyo matakwa ya Watanzania. Lakini,
nilieleza hofu yangu kuhusu mapendekezo ya Tume na kuwataka Wajumbe wafanye
kazi ya ziada kuondosha udhaifu iwapo wataukubali muundo unaopendekezwa. Nilieleza nia yangu ya kutaka tuwe na
Serikali ya Muungano yenye ukuu unaoonekana, yenye nguvu ya kuweza kusimama
yenyewe, inayoweza kuwa tegemeo kwa nchi Washirika, Serikali isiyokuwa tegemezi
wala egemezi kwa nchi washirika na ambayo inavyo vyanzo vya uhakika vya
mapato. Hivi kwa kutoa ushauri huo kwa
Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba inageuka kuwa nongwa. Kwa kweli sielewi lawama ni ya nini?.
Naamini sistahili lawama bali pongezi
kwa kuwa muwazi na kutoa ushauri wa msingi ambao utasaidia nchi kupata Katiba
nzuri inayojali maslahi ya watu wa nchi yetu na ya nchi zetu mbili zilizoungana
miaka 50 iliyopita.
Na Mwanaharakati.
No comments:
Post a Comment