MAC PRODUCTION STUDIO'S

MAC PRODUCTION STUDIO'S
KWA MATANGAZO YA BIASHARA REDIONI( 0767-814844)

Friday, 14 September 2012

PINDA KUMALIZA TATIZO LA MAJI MAGU


WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda amesema atalimaliza tatizo la maji katika mji mdogo wa Magu ili kuwaondolea shida hiyo wakazi wake ambao kwa sasa ni asilimia 17 tu wanaopata maji safi.
Akihutubia mkutano wa hadhara mjini Magu katika siku yake ya pili ya ziara ya wiki moja ya mkoa wa Mwanza leo (Alhamisi Sept. 13, 2012) alisema yuko radhi kufanya kila atakaloliweza ili tatizo la maji Magu linamalizwa.
“Sitaki nirudi hapa mnambie kwamba ahh… nawe kumbe ni bomu tu…mimi sikubali kuitwa bomu. Nikirudi Dar es Salaam kazi yangu ni moja tu, maji ya Magu,” aliuambia umati wa wananchi waliokuwa wanamsikiliza.
Alisema, kwanza atafanya kila njia kupata Sh. Milioni 200 kwa ajili ya kurekebisha mifumo ya maji ili angalau asilimia 30 ya watu wapatao 38,000 (watu 11,400) wa mji wa Magu wapate maji.
Pili amewaagiza wataalamu kufanya mchanganuo wa kuboresha mfumo wa maji utakaogharibu Sh. Bilioni 8, ili fedha hizo zipatikane awamu kwa awamu na baadaye asilimia 70 ya wakazi hao (watu wapatao 27,000)   wapate maji safi, alisema.
Maji safi ni kilio cha wakazi wa mji wa Magu unaokua kwa kasi, ambao uko karibu na  Ziwa Victoria.  Mahitaji  halisi ya maji mjini Magu ni mita za ujazo zaidi ya 7,000 kwa siku, lakini uzalishaji sasa ni mita za ujazo 1,200 tu.

ATOA SH. MILIONI 15 KWA VIKUNDI VYA VIJANA WATAKAOCHONGEWA MITUMBWI KWA MPANGO WA “KOPA MTUMBWI LIPA MTUMBWI”
 Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu Pinda ameahidi kutoa Sh. Milioni 15 ili kuwakopeshwa vijana wa wilaya ya Magu watakaochongewa mitumbwi ya kuvulia samaki Ziwa Victoria chini ya mpango wa “Kopa Mtumwi, Lipa Mtumbwi” ili wajiajiri wenyewe na kupata kipato.
Alisema aatamkabidhi fedha hizo Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Injinia Evarist Ndikilio, ili vijana watakaojiunga katika vikundi watapatiwa mtumbwi, lakini watalipa mtumbwi ili mpango huo uwe endelevu. Mtumbwi mmoja unagharimu Sh. 300,000/= na kwa fedha hizo itapatikana mitumbwi 50.
Waziri Mkuu aliyasema hayo baada ya kuzindua rasmi gati la kupokelea samaki katika kijiji cha Kigangama ambako aliambia baadhi ya vijana wanaishia kuajiriwa na watu wengine kuvua kwa vile wao hawana mitumbwi.
Mapema alikagua shamba la kilimo cha kisasa cha mboga cha umwagiliaji kinachoendeshwa na mjasiriliamali mzalendo, Nd. Peter Ngongo Seke, katika kijiji cha Nsola.
Waziri Mkuu alitembelea shamba hilo la Ngongo Seke Horticulture Farm, ambalo tayari linazalisha nyanya, matango na pilipili hoho zinazouzwa kwenye migahawa ya machimbo ya madini ya wawekezaji wakubwa pamoja na maduka makubwa (supermarkets) Mwanza na Dar es Salaam.
Kilimo hicho kinaendeshwa kitaalamu, kwa kutumia mbolea asilia, bila ya kemikali na kwa umwagiliaji wa teknolojia ya matone, ndani ya mabanda maalum. Kwa kawaida, mboga zinazolimwa kwa mtindo huo huwa zinaagizwa kutoka nje.
Mhe. Pinda alivutiwa sana na shughuli hiyo na kusema angetaka mashamba ya aina hiyo yawe mengi katika wilaya ya Magu, katika Mkoa wa Mwanza na nchini kote.
Waziri Mkuu alikagua mradi wa ufugaji nyuki kisasa na alimtembelea Mwalimu Mbeba, ambaye aliwahi kumfudisha shuleni zamani.
Kesho (Ijumaa Sept. 14, 2012) anaitembelea Wilaya ya Kwimba.
(mwisho)
Imetolewa na:
          Ofisi ya Waziri Mkuu,
          S.L.P. 3021,
          DAR ES SALAAM
Alhamisi Sept. 13, 2012

No comments: