MAC PRODUCTION STUDIO'S

MAC PRODUCTION STUDIO'S
KWA MATANGAZO YA BIASHARA REDIONI( 0767-814844)

Friday, 10 October 2014

NEWS ALERT!!!RAIS KIKWETE AWA MGENI MAALUM KATIKA MIAKA 52 YA UHURU WA UGANDA



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete jana, Alhamisi, Oktoba 9, 2014, amekuwa Mgeni Maalum katika Sherehe za Kuadhimisha Miaka 52 ya Uhuru wa Uganda zilizofanyika kwenye Viwanja vya Sherehe vya Kololo mjini Kampala.

Kwa nafasi yake ya kuwa Mgeni Maalum, Rais Kikwete amekuwa kiongozi pekee mwalikwa kupata nafasi ya kutoa salamu kwa wananchi wa Uganda ambayo Oktoba 9, mwaka 1962, ilipata Uhuru kutoka kwa wakoloni wa Kiingereza.

Viongozi wengine ambao wameshiriki katika sherehe hizo za kufana na zilizohudhuriwa na mamia kwa mamia ya wananchi ni Rais Salva Kiir wa Sudan Kusini, Rais Paul Kagame wa Rwanda, Makamu wa Rais wa Burundi na wawakilishi wa nchi za Kenya na Ethiopia.

Rais Kikwete ambaye aliwasili Uganda mapema jana asubuhi akitokea Dodoma, ambako juzi alipokea Katiba Inayopendekezwa katika sherehe kubwa na ya kufana sana iliyofanyika kwenye Uwanja wa Jamhuri, amekwenda moja kwa moja Uwanja wa Kololo, ambako aliingia dakika mbili kabla ya kuingia kwa mwenyeji wake, Rais Yoweri Kaguta Museveni.

Akimtambulisha Rais Kikwete kwa wananchi waliofurika kwenye Uwanja huo wa Kololo, Rais Museveni aliwaambia wananchi hao: “Hapa mbele yenu mnaona Jeshi imara kabisa la UPDF (Uganda People’s Defence Army) na Jeshi la Polisi lililo imara pia. Nguvu na uwezo huu wa Jeshi na Polisi wetu umejengwa na pande mbili kubwa.”

Ameongeza Rais Museveni: “Upande wa kwanza ni sisi wenyewe wananchi wa Uganda na hili mnalijua vizuri sana. Upande wa pili alikuwa ni Mwalimu Julius Nyerere, Mwanzilishi na Baba wa Taifa la Tanzania. Yeye hatunaye tena, yeye sasa amekuwa Omugenzi, yaani ametangulia, kama sisi sote tutakavyokwenda. 

Hata hivyo, leo tunaye mmoja wa viongozi wa Tanzania ambao wamemfuatia Mwalimu Nyerere katika uongozi wa nchi hiyo, naye ni Rais Kikwete. Karibu Rais Kikwete uzungumze na wananchi wa Uganda.”

Akizungumza kwa ufupi tu na wananchi hao, Rais Kikwete amewaambia wananchi hao: “Ndugu zangu wananchi wa Uganda, nawaleteeni salamu nyingi za kindugu na kirafiki kutoka kwa ndugu zenu wa Tanzania. Wamenituma niwaletee salamu nyingi za pongezi katika kuadhimisha miaka 52 ya Uhuru wa nchi yenu.”

Rais Kikwete aliwapongeza wananchi wa Uganda kwa mafanikio makubwa ambayo yamepatikana tokea Uhuru na hasa katika miaka 28 ya uongozi wa Rais Museveni. 

“Mwenye macho haambiwi tazama na mwenye masikio haambiwi sikia. Kama kuna mtu haoni maendeleo dhahiri kabisa ambayo yamepatikana chini ya uongozi wa Rais Museveni basi ana lake jambo ama hataki tu kuambiwa, kutambua na kukubali ukweli.”

“Chini ya uongozi imara wa Rais Museveni, Uganda imefanikiwa kurejesha amani na utulivu, jambo ambalo kuna wakati lilipotea kabisa katika nchi hii madhubuti.  Kwa niaba ya wananchi wa Tanzania, napenda kukupongeza wewe Mheshimiwa Museveni na wananchi wote wa Uganda kwa mafanikio haya,” amesema Rais Kikwete.

Rais Kikwete ambaye amefuatana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mheshimiwa Bernard Membe, ameondoka Uganda mara baada ya kumalizika kwa sherehe hizo kwenda Mwanza, ambako atafanya ziara ya siku mbili kukagua shughuli za maendeleo katika mkoa huo.

Na Mwanaharakati.

No comments: