MAC PRODUCTION STUDIO'S

MAC PRODUCTION STUDIO'S
KWA MATANGAZO YA BIASHARA REDIONI( 0767-814844)

Monday, 18 August 2014

NEWS ALERT!!! TANZANIA HAKUNA EBOLA

Mtaalam wa ufuatiliaji wa magonjwa ya binadamu wa wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii Dkt. Vida Mmbaga akitoa ufafanuzi kuhusu historia ya ugonjwa wa Ebola, Virusi vyake , dalili na namna unavyoenea wakati wa mafunzo maalum kwa waandishi wa habari kuhusu ugonjwa huo jijini Dar es salaam.


Imeelezwa kuwa Tanzania kwa sasa haina  raia yeyote  aliyeingia nchini kutoka mataifa mengine aliyebainika kuwa na maabukizi ya Virusi vya ugonjwa wa Ebola kufuatia zoezi linaloendelea la uchunguzi wa wasafiri wanaoingia nchini kupitia viwanja vya ndege na maeneo mengine.

Hayo yamebainishwa kwa nyakati tofauti na wataalam wa ufuatiliaji wa magonjwa ya binadamu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii wanaoshughulikia magonjwa ya milipuko wakati wa mafunzo kuhusu ugonjwa  wa Ebola kwa waandishi wa habari jijini Dar es salaam.

Wamesema kuwa ugonjwa huo licha ya kuleta madhara na maafa makubwa katika maeneo ya nchi za Afrika Magharibi kama zinavyoonyesha taarifa za Shirika la Afya la Umoja wa Mataifa (WHO) bado haujaingia nchini Tanzania na kuongeza kuwa tayari Serikali kupitia wizara ya Afya imechukua  hatua za udhibiti  kupitia timu ya wataalam wa afya walio katika maeneo mbalimbali nchini.


Dkt. Chacha Mung’aho ambaye ni Afisa Afya Mkuu kutoka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii anayeshughulikia maeneo ya Bandari, Viwanja vya ndege na mipakani akizungumzia namna walivyojipanga kukabiliana na tishio la ugonjwa wa Ebola  kupitia wasafiri wanaoingia nchini Tanzania amesema kuwa  tayari Serikali imetenga maeneo maalum, vifaa vya uchunguzi na huduma kwa wasafiri watakaobainika kuwa na dalili za maambukizi ya ugonjwa huo.

Amesema kuwa wataalam waliopo kutoka Wizara ya Afya wanaendelea  kushirikiana na wenzao wa Mamlaka ya Viwanja vya ndege, Uhamiaji na Wizara ya Kilimo na vyombo vingine vya ulinzi na usalama ili kuendesha zoezi la uchunguzi wa afya ili kupata taarifa za wasafiri kulingana na mataifa wanayotoka.

“Kwa sasa tunafanya kazi kwa kushirikiana na tunapata taarifa sahihi za abiria kutoka kwa mashirika ya ndege wanayotumia kusafiria jambo linalotusaidia kuwabaini wasafiri waliotoka katika nchi za Liberia, Ivory Coast na Guinea zilizoathiriwa na ugonjwa huo” Amebainisha Dkt. Chacha.

Amesema tangu kugunduliwa kwa ugonjwa huo mwezi Machi mwaka huu huko Afrika Magharibi mataifa  mbalimbali duniani kote yamekuwa katika mapambano kudhibiti ugonjwa huo kuendelea kusambaa na kuleta maafa katika maeneo mengine duniani ambako haujafika.

Afisa Afya Mkuu kutoka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii anayeshughulikia maeneo ya Bandari, Viwanja vya ndege na mipakani Dkt. Chacha Mung’aho  akizungumza namna walivyojipanga kukabiliana na tishio la ugonjwa wa Ebola  kupitia wasafiri wanaoingia nchini Tanzania.


Amesema serikali kupitia Wizara ya Afya inaendelea kutoa elimu kwa wananchi kupitia vyombo vya habari juu ya namna ya kujikinga na kuchukua tahadhari na  endapo watabaini uwepo wa mtu mwenye dalili za Ebola pia kuratibu mipango yote ya vifaa tiba,matibabu na mazishi endapo ugonjwa huo utaingia nchini kupitia kamati ya maafa ya Ofisi ya Waziri Mkuu .

Aidha, amesema licha ya ugonjwa huo kuibuka na kupotea katika vipindi tofauti katika mataifa mengine ya bara la Afrika na nchi jirani  za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Uganda , wataalam hapa nchini wanaendelea kufanya utafiti juu ya chanzo kinachohifadhi Virusi hao kutokana na tabia yao ya kupotea katika kipindi fulani na kuibuka tena.
 Na Mwanaharakati.

No comments: