MAC PRODUCTION STUDIO'S

MAC PRODUCTION STUDIO'S
KWA MATANGAZO YA BIASHARA REDIONI( 0767-814844)

Thursday, 15 January 2015

BALOZI WA ALGERIA NCHINI AONDOKA KWA MASIKITIKO



Balozi wa Algeria ambaye aliyemaliza muda wake wa utumishi katika Tanzania, Mheshimiwa Tabat Jallouh amewatakia Watanzania mwaka wa mafanikio, amani na utulivu wa 2015, kwa kadri nchi inavyopitia katika mabadiliko makubwa ya kisiasa kwa njia ya kura ya maoni ya Katiba Mpya na Uchaguzi Mkuu.

Mheshimiwa Jallouh alitoa salamu zake hizo kwa Watanzania  Jumatano, Januari 14, 2015, wakati alipokuwa anaagana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Ikulu, Dar es Salaam.

Balozi Jallouh alimwambia Rais Kikwete kuwa anasikitika kuondoka mapema bila kuwa shuhuda na shahidi wa matukio hayo muhimu katika historia na uhai wa taifa la Tanzania.  
   
“Nakutakia wewe binafsi, Mheshimiwa Rais na kupitia kwako, Watanzania wote, mwaka wenye utulivu, mafanikio na amani kwa kadri nchi inavyopita kipindi cha kutunga Katiba Mpya na Uchaguzi Mkuu. Ni matukio muhimu sana katika historia na uhai wa taifa la Tanzania,” alisema Balozi Jallouh, ambaye pia alimtakia Rais Kikwete maisha marefu na shughuli zenye mafanikio baada ya kustaafu.

Balozi Jallouh ambaye Tanzania ilikuwa nchi ya kwanza Kusini mwa Jangwa la Sahara kuitumikia katika utumishi wake wa kibalozi, amekuwa Balozi wa Algeria katika Tanzania kwa miaka mitano.

Naye Rais Kikwete amemshukuru Balozi Jallouh kwa kuinua kwa kiwango kikubwa uhusiano wa Tanzania na Algeria. “Tunakushukuru kwa utumishi wako, tunakushukuru kwa kutuunga mkono, tumekuwa marafiki wa miaka mingi lakini wewe umetoa mchango wa pekee. Tutakukumbuka daima.”
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.
14 Januari, 2015
 

Na Mwanaharakati.

No comments: