MAC PRODUCTION STUDIO'S

MAC PRODUCTION STUDIO'S
KWA MATANGAZO YA BIASHARA REDIONI( 0767-814844)

Saturday, 18 July 2015

HATIMAYE HUDUMA YA WAGONJWA MAHUTUTI KAGERA YASOGEZWA KARIBU.



Ni baada ya jengo lenye wodi mbili kwa ajili wanawake na wanaume kuelekea kukamilika ujenzi wake katika hospitali ya rufaa ya mkoa katika manispaa ya Bukoba linalotarajia kugharimu zaidi ya shilingi milioni 95 na litakuwa na uwezo wa kuwahudumia wagonjwa wanane kwa wakati mmoja. 

Ni jengo la wodi ya wagonjwa mahututi (Intensive Care Unit) katika hospitali ya rufaa mkoa Kagera litakalokuwa likitoa huduma kwa wagonjwa mahututi bila kujali jinsi kutokana na uhitaji wake, ambapo wananchi wamekuwa wakikosa huduma hiyo na kutajwa kupoteza maisha hata kama ingewezekana wakatibiwa.

Akikagua jengo hilo ambalo limefikia asilimia 99% katika ujenzi wake katibu tawala wa mkoa  Kagera Bw. Nassor Mnambila Bw. Mnambila alisema kuwa serikali ya mkoa iliamua kujenga jengo hilo la wagonjwa mahututi ambalo hapo mwanzo halikuwepo na wagonjwa mahututi kukosa huduma ya sehemu maalum ya uangalizi wa karibu na kusababisha usumbufu mkubwa kwao ambapo amesisitiza likamilishwe kwa muda uliopangwa ili lianze kutumika na kutoa huduma kwa wananchi.

Aidha akiongea na uongozi wa hospitali hiyo Bw. Mnambila alitoa changamoto kwao kuwa sasa ni wakati wa serikali kushirikiana na sekta binafsi katika kutekeleza miradi ya maendeleo inayowagusa wananchi moja kwa moja badala ya kuitegemea serikali tu ambapo aliwashauri kuandika maadiko ya miradi mbalimbali na kuiuza kwa sekta binafsi na mashirika yasiyokuwa ya serikali.

Kutokana na maeneo ya hospitali hiyo kuonekana kuwa finyu kwasababu ya kujenga majengo mbalimbali ya chini aliwashauri kuona uwezekano wa kujenga majengo ya kwenda juu ambayo ni maghorofa kwasababu itafika mahali hakuna tena sehemu ya kujenga jengo lolote kutokana na ufinyu wa ardhi.
Mganga Mkuu wa Mkoa Dk. Thomas Rutachunzibwa akimshukuru Katibu Tawala Mkoa Bw. Mnambila alisema anamshukuru yeye binafsi na serikali kwa ujumla kuona umuhimu  wakujenga jengo la wagonjwa mahututi katika Hospitali ya Rufaa ya mkoa na kupunguza usumbufu waliokuwa wanaupata, lakini mara baada ya jengo hilo kukamilika litaondoa tatizo hilo.
 
Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Kagera inawahudumia wastani wa wagonjwa 12,000 kwa mwezi na wastani wa wagonjwa 150,000 kwa mwaka ambapo mwaka 2013 iliwahudumia wagonjwa 151,915 na mwaka uliofuata iliwahudumia wagonjwa 156,376. Lengo kubwa la Sekretarieti ya mkoa wa Kagera ni kutoa huduma nzuri kwa wananchi wake. 

Na Mwanaharakati.

No comments: